RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali
Mohamed Shein amewataka wananchi kuacha ukaidi na kufuata kikamilifu maelekezo ya Serikali, ikiwa ni hatua za kuunga mkono juhudi za Serikali katika kukabiliana na Virusi vya Ugonjwa wa Corona.
Dk. Shein amesema hayo Binguni Mkoa wa Kusini Unguja, alipolitembelea
eneo linalojengwa Hospitali kuu ya Kisasa, mahala ambapo pia itajengwa Taasisi ya Utafiti ya Wizara ya Afya.
Amesema katika kukabiliana na virusi vya ugonjwa huo, Serikali tayari
imetowa malekezo kadhaa, ikiwa njia ya kujikinga na virusi vya ugonjwa huo, hivyo akawataka wananchi kuacha ukaidi na kutekeleza maelekezo ya kudumisha usafi kama inavyoelekezwa.
Alisema Virusi vya Ugonjwa wa Corona ni janga la Kimataifa na ni maradhi
yasiotaka mzaha wala hayachaguwi aina ya mtu wa kuamuathiri, hivyo ni vyema wananchi wakaondokana na ushindani na kuzingatia maelekezo ya Serikali.
Alieleza kuwa Serikali imeingia katika vita dhidi ya adui asieonekana na
hivyo ikalazimika kuchukuwa hatua mbali mbali za dharura ikiwemo kuzuia Kongamano la dini pamoja na kuzifunga skuli zote na wanafunzi kukosa taaluma.
Shein alisema Serikali haiwezi kuainisha ukubwa wa gharama
inazopoteza kutokana na hatua ilizochukuwa katika kukabiliana na virusi vya ugonjwa wa Corona, sambamba na athari za kiuchumi zitokanazo na kuvurugika kwa sekta ya utalii, ambayo huchangia asilimia themanini ya Pato la Taifa. Rais Dk. Shein aliwataka wananchi kuondokana na upotoshaji kupitia mitandao ya kijamii.
Aidha, alisisitiza umuhimu wa wananchi kuondokana na mikusanyiko,
hususan katika eneo la Hospitali kuu ya Mnazi mmoja pamoja na maeneo ya masoko, kwa kigezo kuwa hatua hiyo inaweza kuwa chanzo cha kusambaa kwa viusi hivyo, pale itakapotokezea mtu mmoja kuwa navyo.
Katika hatua nyengine, Dk. Shein alilisistiza azma ya Serikali ya kujikita
katika kufanya uchunguzi wa maradhi mbali mbali kwa kigezo kuwa hakuna tiba muafaka bila ya kuwepo uchunguzi, hivyo akabainisha dhamira ya Serikali katika kukamilisha ujenzi wa jengo la kisasa la Maabara katika eneo hilo la Binguni.
Alisema Serikali imefikia uamuzi wa kukamilisha jengo hilo mahala hapo
kwa kuzingatia mazingira bora yaliopo, ambayo yamejitenga na eneo la makaazi ya wananchi.
Aliwahakikishia wananchi kuwa jengo hilo litakamilika katika kipindi kifupi
kijacho na kuwekewa vifaa vyote muhimu ili kukidhi mahitaji na malengo yaliokusudiwa.
Aidha, alisema Serikali itakamilisha miradi yote ya Maendeleo iliyokwisha
anzishwa, ikiwemo ya ujenzi wa Nyumba Kwahani, Michenzani Moull, Barabara, Mahakama Kuu na mingineyo pamoja na kuanzisha miradi mipya, huku akibainisha kuwa endapo kutatokezea upungufu wa fedha itaangalia namna ya kukamilisha miradi hiyo.
Mapema, Waziri wa Afya Hamad Rashid Mohamed, amesema Wizara hiyo
imejiandaa kikamilifu kushirikiana na Serikali ya Watu wa China katika dhana ya kukuza utalaamu ili kuleta ufanisi wa maabara itakayojengwa.
Abdi Shamna, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777476982. Fax: 024 2231822