You are on page 1of 3

JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA

OFISI YA MAKAMU WA RAIS


Anwani ya simu: MAKAMU,
Simu Na. +255 2116919
Fax Na. +255 2116990

Barabara ya Luthuli,
P.O Box 5380,
Dar es Salaam.

Barua Pepe: km@vpo.go.tz

TANZANIA.
22/04/2016

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

Makamu wa Rais Samia Suluhu Hassan amezitaka nchi za Maziwa Makuu na


Pembe ya Afrika kuanza utaratibu wa kuziweka alama silaha ndogo ndogo ili
kufanikisha azma ya nchi hizo ya kudhibiti tatizo la kuzagaa kwa silaha
haramu.
Samia ametoa kauli hiyo leo kwenye ufunguzi wa mkutano wa mawaziri wa
nchi wanachama wa Taasisi inayopambana na tatizo la Silaha haramu katika
nchi za Maziwa Makuu na Pembe ya Afrika (RECSA) uliofanyika leo katika
hoteli ya Naura Spring mjini Arusha
Alisema utaratibu huo utasaidia kuzitambua silaha hizo zinatoka nchi gani
endapo zitakamatwa na kuziharibu zisizokuwa na alama ili zisirudi tena
mikononi mwa wananchi na kubainisha kuwa Tanzania tayari imeanza zoezi
hilo.
"Jambo jingine ambalo nimetilia mkazo ni kuzitaka nchi zetu kuziweka alama
silaha ndogo ndogo. Tanzania tumeanza zoezi hili....zoezi hili linasaidia silaha
yoyote ikikamatwa, tutajua inatoka nchi gani, kwa hiyo inakuwa rahisi
kuziharibu zisizokuwa na alama zisirudi mikononi kwa wananchi," alisema
Makamu wa Rais
Alisema kuenea kwa silaha ndogo ndogo katika nchi hizo kumechochea
makosa mbalimbali ya jinai yakiwamo ugaidi, ujangili, wizi wa kutumia silaha,
uharamia na kuwafanya
wananchi washindwe kufanya shughuli za
maendeleo.

Makamu wa Rais aliueleza mkutano huo kuwa inakadiriwa silaha ndogo


ndogo zipatazo milioni 875 zimezagaa duniani kote na kati ya hizo asilimia
75 zinamilikiwa na raia iwe kihalali ama siyo kihalali ambapo zaidi ya milioni
100 ya silaha hizo zinapatikana Afrika.
"Nyingi ya silaha hizo zinaingizwa kwenye soko haramu na kwa hiyo
huchangia kudhoofisha amani na usalama, inapunguza upatikanaji wa
huduma za jamii na hatimaye ni kurudisha nyuma maendeleo," alisema
Samia.
Alisema amepata taarifa kuwa watu wasio na hatia wapatao 1,000 wanakufa
kila siku na kati ya watu 300,000 na 500,000 wanakufa kila mwaka duniani
kote kwa matumizi mabaya ya silaha ndogo ndogo.
Aliongeza kusema kuwa nchi zinazotengeneza silaha, hutengeneza kati ya
silaha milioni 7 hadi 8 kwa mwaka huku silaha chache zikiharibiwa jambo
ambalo linapelekea kuongezeka kwa idadi ya raia wanaomiliki silaha haramu
na sambamba na kuzagaa kwa silaha hizo.
Aliwataka mawaziri hao kutafuta ufumbuzi wa kudumu na kuweka mikakati
itakayowezesha kufichua na kuving'oa vikundi vya watu vinavyoendesha
biashara haramu ya silaha ndogo ndogo bila ya kujali hadhi na nafasi
walizonazo katika jamii.
"Watu watakaobainika kufanya biashara haramu ya silaha washughulikiwe
bila ya kuonewa huruma ikiwa ni pamoja na kufikishwa Mahakamani ili haki
siyo tu itendeke lakini pia ionekane," alisema Samia.
Alisisitiza umuhimu wa kuingiza wanawake katika harakati za kupambana na
tatizo la silaha haramu kwa kuwa wanawake ndiyo wanaoathirika zaidi na
migogoro ya kivita na wana uwezo mkubwa wa kuleta amani katika nchi zao.
Mkutano huo unatarajia kuchagua Mwenyekiti mpya baada ya Tanzania
kumaliza muda wake na pia Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi hiyo ya RECSA.
Imetolewa na
Ofisi ya Makamu wa Rais
Dar es salaam
22/4/2016

You might also like