Serikali ya Urusi imeahidi kuongeza fursa za masomo ya elimu ya juu kwa wanafunzi wanaotoka Tanzania. Ahadi hiyo imetolewa na Waziri wa Viwanda na Biashara wa Urusi, Denis Manturov wakati alipokutana na Makamu wa Rais Samia Suluhu Hassan, leo Ikulu, ambapo alimkabidhi ujumbe wa Rais John Magufuli kutoka kwa Rais Vladmir Putin wa Urusi. Alisema serikali yake kwa mwaka jana ilitoa nafasi kumi kwa wanafunzi wanaotoka Tanzania kujiunga na vyuo vya elimu ya juu nchini Urusi na kwamba wameahidi kuongeza idadi ya wanafunzi watakaofaidika na masomo Urusi. Manturov alitumia fursa hiyo kumweleza Makamu wa Rais kuwa Warusi wako tayari kuwekeza hapa nchini katika sekta mbalimbali zikiwemo za kilimo, viwanda, utalii, nishati, mafuta na gesi. Katika mazungumzo hayo, Makamu wa Rais alimweleza Waziri huyo kwamba Tanzania ina fursa nyingi za uwekezaji na kusema upande wa mafuta na gesi serikali itaangalia maeneo muafaka kwa Urusi kujenga viwanda. Akizungumzia mapendekezo ya kuanzishwa kwa Tume ya Pamoja ya Ushirikiano kati ya Tanzania na Urusi Samia alimwakikishia Waziri huyo kwamba Mkataba wa Makubaliano waliouleta unapitiwa na Wizara ya Mambo ya Nje kwa ajili ya kukamilisha taratibu za kisheria katika ushirikiano huo. Alisema Tume hiyo ni muhimu katika kudumisha na kuimarisha mahusiano ya muda mrefu ya kiuchumi na kijamii kati ya nchi hizo mbili. Katika suala la utamaduni Makamu wa Rais alishauri mafunzo ya lugha za kiswahili na Kirusi yatolewe kwa pande zote mbili ili hatimaye yarahisishe sekta ya utalii. Imetolewa na