You are on page 1of 7

HOTUBA YA MHE.

BAHAME TOM NYANDUGA, MWENYEKITI WA TUME


YA HAKI ZA BINADAMU NA UTAWALA BORA WAKATI WA UZINDUZI WA
TAARIFA YA UCHUNGUZI KUHUSU KUZUIA MATANGAZO YA MOJA KWA
MOJA YA SHUGHULI ZA BUNGE. NCHI YETU, BUNGE LETU. JOSAM
GARDENS, MWENGE, DAR ES SALAAM
15 NOVEMBA 2016
Ndugu wajumbe wa Bodi ya Baraza la Waandishi wa Habari Tanzania,
Ndugu Katibu Mtendaji wa Baraza la Waandishi wa Habari Tanzania,
Ndugu waandishi wa habari mliopo, wageni waalikwa, mabibi na mabwana,
Aslaam Aleykum, habari za asubuhi.

Napenda kutoa shukrani za dhati kwa niaba ya Tume ya Haki za Binadamu na


Utawala Bora, na kwa niaba yangu binafsi, kwa mwaliko wenu.
Napenda kusema kuwa nimefurahi kushirikishwa katika matukio mawili
muhimu katika kazi yenu ya uandishi wa habari, ambayo ni uzinduzi wa
Taarifa ya uchunguzi kuhusu zuio la matangazo ya moja kwa moja ya
shughuli za Bunge, na pia kuzindua mchakato wa shindano la kutafuta
washindi wa Tuzo za waandishi wa habari Mahiri katika maeneo 23, ambayo
Baraza na tasnia ya habari kwa ujumla, mmeyaanisha.
Madhumuni ya mchakato huu ni kutafuta waandishi wa habari ambao
wamejipambanua katika kutoa habari mbalimbali, kupitia vyombo mbalimbali
vya habari vilivyopo nchini, yaani kupitia magazeti, runinga, na radio, ama
kwa kupitia makala, picha na hata vibonzo katika kufikisha ujumbe kwa jamii.
Napenda niseme awali kwamba tasnia ya habari ni kitu muhimu sana katika
jamii na nchi yoyote ile, katika kutekeleza majukumu yake. Niseme pia
kwamba katika nchi yenye kuamini katika demokrasia, tasnia ya habari ni
mojawapo ya nguzo muhimu ya uwepo wa demokrasia ya kweli, kwani
huwezesha wananchi kujua kile kinachotokea nchini, na katika jamii wakati
wote kupitia uwezo wake wa kuelemisha jamii. Kwa maana hiyo wananchi
hupata taarifa nyingi wakiamini kwamba taarifa au habari hizo ni sahihi, na
kwamba waandishi wa habari wanafanya kazi yao kwa weledi, na kwa
umakini ili kuhakikisha kuwa habari zinazowafikia wananchi zinakuwa
zimefanyiwa utafiti, uchunguzi, na uchambuzi wa kutosha. Kwa hiyo ni
lazima waandishi wa habari kuwa na vyanzo vya habari vinavyoaminika, na
1

wasitoe habari za uzushi au za kubuni, ili taaluma ya uandishi wa habari


iheshimike. Na huo ndiyo uweledi na umahiri pamoja na kujikita katika
maadili ya kazi.
Katika misingi muhimu ambayo imetokea kutambulika kama vielelezo vya
Utawala Bora ni pamoja na hii ifuatayo, demokrasia, uwajibikaji, uwazi,
utawala wa sheria, uheshimu wa mgawanyo wa madaraka kati ya mihimili
ya dola- yaani uhuru wa mahakama, (Judiciary,) uhuru wa Bunge
(Parliament,) uhuru wa Mhimili wa Utendaji, yaani serikali (kwa maana ya
executive branch,) na uhuru wa vyombo vya habari.
Pamoja na misingi hiyo, umuhimu wa mihimili mikuu mitatu ya dola kufanya
kazi kwa kujali mipaka ya mhimili mwingine, ndiyo unaojulikana katika dhana
ya kikatiba ya utenganifu wa mihimili au heshima baina ya mihimili, (yaani
separation of powers.) Katika utendaji wake kila mhimili hufanya kazi kwa
kuangalia ukomo wa mipaka yake bila kuathiri utendaji wa mhimili mwingine
yaani (checks and balances,) nia ya
mfumo huu katika utendaji ni
kuhakikisha mhimili mmoja usiwe na nguvu kuliko mhimili mwingine.

Inapotokea kwa mfano mhimili wa serikali (Executive branch) inapovuka


mipaka yake ya sheria na kusababisha uvunjifu wa haki za binadamu basi
mhimili wa Mahakama (Judiciary) una uwezo wa kupitia uhalali wa matendo
ya serikali au sheria husika na kutolea maamuzi (Judicial Review). Na huu
ndio msingi mkubwa wa utawala wa Sheria unaoamini katika kila mtu au
taasisi kuwajibika ndani ya sheria (Rule of Law.)
Misingi hii ya utawala bora na misingi ya uheshimu wa separation of powers
hushabihiana. Ni vigumu kuwa na demokrasia kamilifu iwapo mmoja wapo
wa misingi hiyo hautakuwepo. Kama nilivyosema hapo awali katika
demokrasia, msingi wowote katika hiyo misingi ikikosekana, lazima
kunatokea mapungufu katika mustakabali mzima wa demokrasia.
Ingawaje tasnia ya habari si mhimili, lakini imeonekana kuwa ndiyo gundi
inayounganisha mihimili hiyo na jamii kwa ujumla, kwa kuwa kila
kinachofanyika kwenye mhimili mmoja wapo, na kikabaki ndani bila kutolewa
nje kama habari, basi wananchi au jamii haitafahamu kile kinachofanyika
huko ndani. Ndiyo sababu katika kila tukio litokeapo, linalohusu habari katika
mhimili mmoja wapo, lazima pawepo na wandishi wa habari, wakitumia
taaluma yao ili kufikisha ujumbe wa kile kilichotendeka kwa jamii kwa
ujumla. Ni kutokana na umuhimu wa tasnia ya habari ndiyo sababu kuna
2

wengine wamediriki hata kuuita mhimili wa nne wa dola au kwa lugha ya


kigeni, the Fourth Estate.

Naamini baada ya kuyasema hayo tutaona ya kwamba, na naamini


tunakubaliana wote kwamba ili tasnia ya habari iweze kufanya kazi zake kwa
ufanisi zaidi, upatikanaji wa habari, uenezi wa habari na umuhimu wa kila
mtu kupata habari na kuwa na maoni tofauti katika masuala mbalimabli
katika jamii, ulitambuliwa na Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa mnamo mwaka
1948 katika Azimio la Ulimwengu la Haki za Binadamu, kuwa uhuru wa
habari na maoni ni moja ya haki za msingi za Binadamu, pale Azimio hilo
lilipotamka kwenye Ibara ya 19 kwamba
kila mtu atakuwa na haki ya
kupata habari bila kubughudhiwa, atakuwa na haki ya kujieleza, kutafuta na
kupokea habari, kutoa taarifa na habari, bila mipaka, kupitia matamshi,
maandishi, machapisho, au kupitia sanaa, au njia yoyote ile ya mawasiliano
kwa masharti ya mujibu wa sheria, ili kulinda hadhi na haki ya watu wengine,
kulinda usalama wa taifa, amani na afya ya jamii na maadili, kwa ufupi huu
ndiyo msingi wa haki ya uhuru wa kujieleza na maoni (Freedom of Expression
and Opinion).

Maudhui hayo pia yaliingizwa kwenye Ibara ya 19 ya Mkataba wa Umoja wa


Mataifa wa Haki za Kiraia na Kisiasa wa mwaka 1966. Tanzania ililikubali
Azimio la Umoja wa Mataifa la Haki za Binadamu mara tu tulipopata uhuru,
na pia imeridhia mkataba huu wa haki za kiraia na kisiasa, na inawajibika
kuutekeleza.
Ili kufafanua maudhui ya Ibara ya 19 ya Mkataba wa Haki za Kiraia na Kisiasa
kwa undani zaidi, Kamati ya Haki za Binadamu ya Umoja wa Mataifa (yaani
Human Rights Committee) imefafanua mambo kadhaa ambayo ni muhimu
kuzingatiwa na kila nchi mwanachama.
Katika tamko lake la mwongozo namba 34 kuhusu haki ya uhuru wa kujieleza
na maoni, lililotolewa katika kikao chake cha 102 kilichokutana Geneva
tarehe 11 hadi 29 Julai 2011, Kamati ilisema kuwa haki hii ni haki ya msingi
katika maendeleo ya mwanadamu, na ni msingi muhimu wa jamii
iliyo huru na ya kidemokrasia.

Kamati ilisema pia kwamba Uhuru wa kujieleza na maoni ni msingi


muhimu sana katika uwepo wa uwazi na uwajibikaji, ambazo ni
nguzo muhimu katika ulinzi na utetezi wa haki za binadamu.

Kamati ilitamka pia kwamba maudhui ya haki hii yanatakiwa kuheshimiwa na


mihimili yote ya nchi mwanachama, na kwamba sheria yoyote itakayoweka
kuhusu jinsi ya kutekeleza haki hii lazima iheshimu miongozo inayotolewa na
Kamati hii, ambayo ndiyo yenye mamlaka ya kutafsiri maana ya haki ya
uhuru wa kujieleza na maoni.

Tunafahamu pia kwamba haki hii ya kujieleza na maoni imetamkwa pia


katika Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977 katika
Ibara ya 18 kama haki ya msingi inayolindwa kikatiba hapa nchini.
Ndugu wajumbe wa Bodi ya Baraza, na wageni waalikwa, napenda niombe
kila mwenye nafasi apitie Tamko la mwongozo namba 34 uliyotolewa na
Kamati ya Haki za Binadamu ya Umoja wa Mataifa, kwani muda hauruhusu
kupitia kila lililomo. Kamati inachambua mambo mengi yakiwemo nafasi ya
vyombo vya habari mbalimbali. Kamati inasema kuwa tasnia ya habari iliyo
huru ni nguzo kuu katika demokrasia. (It constitutes one of the cornerstones
in a democratic society.)
Kamati inatambua wajibu wa vyombo vya habari kupokea taarifa na
kuzifikisha kwa wananchi na inasema;
..The free communication of information and ideas about public and
political issues between citizens, candidates and elected representatives is
essential. This implies a free press and other media able to comment on
public issues without censorship or restraint and to inform public
opinion. The public also has a corresponding right to receive media output.
(msistizo umeongezwa)
Kwa ufupi Kamati inasema kuwa vyombo vya habari vinapopata taarifa au
habari zinazohusu jamii au masuala ya kisiasa, vina wajibu wa kuzifikisha
kwa jamii, na wawakilishi wao. Hii ina maana kwamba vyombo vya habari
vilivyo huru vina wajibu wa kutoa maoni yao juu ya masuala yanayohusu
umma bila vikwazo vyovyote, na Jamii pia wanahaki ya kuarifiwa taarifa au
habari hizo kupitia vyombo vya habari.

Kuhusu masharti yanayoweza kuwekwa na sheria kuhusu uhuru wa kujieleza


na maoni, Kamati inasema kwamba, masharti hayo lazima yatimize vigezo
vya ulazima na uuwiano (necessity and proportionality) wa uwepo
wa masharti hayo.
Kamati inasema, nanukuu;
Paragraph 3 may never be invoked as a justification for the muzzling of any
advocacy of multi-party democracy, democratic tenets and human rights.
Nor, under any circumstances, can an attack on a person, because of the
exercise of his or her freedom of opinion or expression, including such forms
of attack as arbitrary arrest, torture, threats to life and killing, be compatible
with article 19. Journalists are frequently subjected to such threats,
intimidation and attacks because of their activities. So too are persons who
engage in the gathering and analysis of information on the human rights
situation and who publish human rights-related reports, including judges and
lawyers. All such attacks should be vigorously investigated in a timely
fashion, and the perpetrators prosecuted, and the victims, or, in the case of
killings, their representatives, be in receipt of appropriate forms of redress.
Kamati inasema kwamba, Ibara ya 19(3) ya Mkataba wa Umoja wa Mataifa
wa Haki za Kiraia na Kisiasa, inayotamka uwepo wa masharti kuhusu kulinda
hadhi na haki za wengine, maslahi ya usalama wa taifa na jamii, isitumike
kwa nia ya kudumaza demokrasia na haki za binadamu, ama kutishia uhuru
wa mtu kujieleza, au hata kwa namna yoyote ile, kusababisha mwandishi au
mtu mwingine yeyote anapohusika na ukusanyaji au uchambuzi wa habari
kupigwa, kuteswa, au hata kuuwawa, mambo ambayo hayaendani na haki
inayolindwa chini ya Ibara ya 19. Na ikitokea hivyo basi matukio hayo ya
kijinai yapelelezwe na wahusika kuadhibiwa.

Nimeona niliweke jambo hilo bayana kwa kuwa nimeshitushwa niliposoma


kwenye Taarifa ya Uchunguzi inaposema katika ukurasa wa 10, nanukuu:
However, there was an aura of disappointment as it was noted that while
television is squarely affected by the government ban, it was the print media
that was making a lot of noise in protesting against the move. The position
of media owners is said to be cautious if anything. Senior editors who also
form the leadership of TEF cite reigning fear due to the unpredictability
of the regime for the stance of the owners. (Msisitizo umeongezwa.)

Taarifa ya Kuzuiwa kwa Matangazo ya Moja kwa Moja ya Shughuli za Bunge


ni taarifa iliyosheheni uchunguzi unaonyesha faida na hasara za uamuzi huo.
Ukiondoa suala la gharama ambalo nalo pia limechambuliwa, na kuonekana
kwamba matangazo yangeweza kuendelea kwa kugharamiwa na vyanzo
visivyo vya serikali, kimsingi taarifa inaonyesha uzoefu wa nchi mbali mbali,
kuwa matangazo hayo ni kitu bora kwa jamii. Taarifa hii inaweza kusaidia
viongozi wanaohusika na maamuzi hayo kuona ni jinsi gani uhuru wa maoni
ni muhimu kuliko gharama. Kuna usemi usemao kwamba demokrasia siyo
kitu rahisi, na ili kuijenga ni budi kuigharamia.
Kwa maoni yangu, na ukiangalia haki ya wananchi waliyonayo ndani ya
mikataba ya kimataifa ya haki za binadamu, na ndani ya Katiba ya nchi, haki
ya kupata taarifa mbalimbali na kuwa na maoni ni haki ya msingi, kwani
inawawezesha wananchi kufikia maamuzi katika masuala muhimu
yanayogusa maisha yao ya kila siku.
Kwa hiyo napenda niwapongeze Baraza la Habari Tanzania kwa utafiti na
uchunguzi mlioufanya mpaka kutengeneza ripoti hii ya Nchi yetu, Bunge
Letu.
Lakini pia napenda nitoe tahadhari kwamba iwapo tayari kuna taharuki ya
uoga katika uandishi wa habari kama ambavyo taarifa ya uchunguzi
inavyosema, siamini kama jamii itakuwa inapata taarifa na habari sahihi za
matukio mbali mbali yanayotokea nchini. Kwani iwapo waandishi wa habari
wataaanza kuandika habari ama kwa woga, ama kwa kutumia self
censorship, ni lazima kwamba weledi utapungua, habari zitaandikwa za
kumpendeza msomaji na habari za uchunguzi zenye kuibua maovu
zitapotea, na hatutakuwa na habari za uchambuzi. Kwa maana hiyo
mchakato wa kutafuta wandishi mahiri ili wawanie Tuzo hautafanikiwa, kwani
ubora wa taarifa na habari utapotea, na kwa kiwango kikubwa ubora wa
tasnia ya habari ambao umekuwa kwa kiwango kikubwa tangu baada ya
mfumo wa vyama vingi kuanza utapotea.

Naamini hatutafika huko iwapo tutazingatia misingi ya haki ya uhuru wa


kujieleza na maoni, na pia misingi ya utawala bora. Kwa hiyo basi nichukue
fursa hii kuwashukuru tena Baraza la Habari Tanzania kwa kunialika.
Niwapongeze kwa kutoa taarifa nzuri ya Uchunguzi wa Uamuzi wa Kusitisha
matangazo ya Shughuli za Bunge, Nchi yetu, Bunge Letu, na niwatakie

Mchakato wenye mafanikio katika kuwania Tuzo za Uandishi mahiri,


Excellence in Journalism Award Tanzania (EJAT 2016).
Baada ya kusema hayo, napenda kutamka kwamba taarifa ya Uchunguzi,
Nchi yetu, Bunge Letu imezinduliwa, na Mchakato wa EJAT 2016 umeanza
rasmi.

Dar es Salaam
15 Novemba 2016.

You might also like