You are on page 1of 3

HOTUBA YA MHESHIMIWA DR. HAMISI A.

KIGWANGALA (MB) WAZIRI WA


MALIASILI NA UTALII KWENYE UZINDUZI WA MRADI WA KUENDELEZA
UTALII UKANDA WA KUSINI (REGROW) TAREHE 12 FEBRUARI 2018, IRINGA
Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Makamu wa Rais wa Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania;
Waheshimiwa Mawaziri, Naibu Waziri wa Wizara za kisekta mliopo hapa
Ndugu, Bella Bird, Mkurugenzi Mkazi wa Benki ya Dunia, Tanzania, Burundi,
Malawi na Somalia
Mheshimiwa Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi,
Maliasili na Utalii
Waheshimiwa Wabunge mliopo hapa
Waheshimiwa Mabalozi mliopo hapa
Ndugu Makatibu Wakuu mliopo hapa
Ndugu Makatibu Tawala mliopo hapa
Watalaam wa sekta mbalimbali
Waandishi wa Habari
Mabibi na Mabwana.

Awali ya yote napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutuwezesha kufika hapa
siku hii ya leo. Aidha, ninakushukuru kwa kukubali mwaliko wa kuja kuzindua Mradi
Kuimarisha usimamizi wa Maliasili na Kuendeleza Utalii Ukanda wa Kusini ujulikanao
kama Resilient Natural Resource for Tourism and Growth (REGROW).

Mheshimiwa Makamu wa Rais,

Napenda pia kutoa shukrani za pekee kwa Benki ya Dunia kwa kukubali kutoa Mkopo
wa masharti nafuu kwa ajili ya mradi huu. Namshukuru sana mama Bella Bird,
Mkurugenzi Mkazi wa Benki ya Dunia kwa Tanzania, Burundi, Malawi na Somalia
ambaye leo ameambatana na mama Julia Bucknall, Mkurugenzi wa Mazingira na
Maliasili wa Benki ya Dunia, kwa kutenga muda wao kuja kuungana nasi katika tukio hili
muhimu. Ninawashukuru Waheshimiwa Mawaziri wenzangu, Wakuu wa Mikoa na
Wabunge kwa kukubali kuja kutuunga mkono. Aidha, napenda niwashukuru watalaam
na watendaji wa Wizara na Taasisi zote walioshiriki katika maandalizi na hatimaye
kukamilisha kuanza kwa mradi huu. Napenda niwashukuru sana wadau wa uhifadhi na
utalii na wananchi wa mikoa ya Iringa na Mbeya, kwa ushirikiano wa hali na mali katika
kufanikisha maandalizi ya mradi huu, ambao hatimaye leo utazinduliwa rasmi.

Mheshimiwa Makamu wa Rais,

Sekta ya Utalii ni moja ya sekta za kipaumbele katika uchumi wa Tanzania na imepewa


umuhimu mkubwa katika Mpango wa Taifa wa Miaka mitano 2016-2021. Takriban,
asilimia 20 ya Pato la Taifa linatokana na utalii na robo ya fedha za kigeni zinatokana na
1
utalii. Kwa kiwango kikubwa mchango huu unatokana na utalii unaofanyika Kanda ya
Kaskazini. Kanda ya kusini ambayo ina vivutio vya pekee na vya aina yake haimudu
kuchangia kikamilifu kutokana na changamoto mbalimbali. Baadhi ya changamoto hizo
ni miundombinu hafifu ya barabara na viwanja vya ndege, uharibifu wa maliasili na
mazingira, kuongezeka matumizi yasiyoendelevu ya maliasili, hususan ujangili wa
tembo. Hali hii kwa kiwango kikubwa imeathiri ubora wa vivutio vya utalii.

Mheshimiwa Makamu wa Rais,

Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka mitano na Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha


Mapinduzi (2015) inaiagiza Serikali kufungua fursa za utalii Kanda ya Kusini. Baadhi ya
hatua muhimu zinazopaswa kutekelezwa zinajumuisha kuimarisha miundombinu ya
barabara na viwanja, kuvutia wawekezaji, kuimarisha usimamizi wa maliasili, kuongeza
wigo wa bidhaa za utalii na kuvitangaza vivutio hivyo. Utekelezaji wa hatua hizo
muhimu unalenga kuongeza idadi ya watalii kufikia milioni mbili kwa mwaka ifikapo
mwaka 2020.

Mheshimiwa Makamu wa Rais,

Mradi wa REGROW ni sehemu ya utekelezaji wa ahadi za Serikali ya Awamu ya Tano


katika kufungua maeneo ya vivutio vya utalii Kanda ya Kusini. Mradi huu ambao ulianza
kuandaliwa tangu mwezi Novemba, 2014 na Timu ya Wataalam wa Sekta mbalimbali za
Wanyamapori, Utalii, Maji, Kilimo, Misitu, Maendeleo ya Jamii na Mazingira. Katika
maandalizi ya Mradi huu, Serikali imeshirikiana kwa karibu na Wataalam wa Benki ya
Dunia. Aidha, maandalizi ya Mradi kwa kiwango kikubwa yamehusisha utambuzi wa
changamoto za uharibifu wa maliasili na mazingira, matumizi yasiyoendelevu na
changamoto ya miundombinu kwenye maeneo ya hifadhi. Hivyo, Lengo na majukumu
yaliyopangwa kutekelezwa yataimarisha usimamizi wa maliasili, kuendeleza utalii na
kuboresha maisha ya wananchi.

Mheshimiwa Makamu wa Rais,

Lengo kuu la mradi huu ni kuimarisha usimamizi wa maliasili, kuboresha miundombinu


ya utalii na kuboresha shughuli za kiuchumi za wananchi wa maeneo yanayozunguka
hifadhi za Ruaha, Mikumi, Udzungwa na Kanda ya Kaskazini ya Pori la Akiba la Selous.
Pamoja na jukumu kubwa la kusukuma ukuaji wa sekta ya utalii, mradi huu utaanza
utekelezaji wa mapendekezo ya Kikosi Kazi ulichounda cha kutafuta ufumbuzi wa
uharibifu wa mazingira na vyanzo vya maji vya mto Ruaha Mkuu. Kukauka kwa Mto huu
kwa siku 60 kwa mwaka kunasababisha wanyamapori kuvamia maeneo ya wananchi na
kuongeza migogoro baina ya wananchi na hifadhi. Mradi wa REGROW utaimarisha
usimamizi wa vyanzo vya maji, matumizi mbalimbali ya maji. Kwa mfano, katika Nyanja
ya kilimo cha umwagiliaji, Mradi umepanga kujenga miundombinu ya umwagiliaji, hivyo
kuwezesha matumizi endelevu ya maji hususani ndani ya hifadhi ya Taifa Ruaha na
uzalishaji wa umeme katika bwawa la Mtera.

Mheshimiwa Makamu wa Rais,

Kupitia mradi wa REGROW, Serikali itajenga na kuimarisha miundombinu ya barabara,


viwanja vya ndege, vituo vya ulinzi wa wanyamapori, na mageti ya kisasa ya kuingilia
2
hifadhini. Kazi hii itatekelezwa ndani ya Hifadhi za Taifa za Ruaha, Mikumi na Udzungwa
na Pori la Akiba Selous. Hivi sasa maeneo mengi ya hifadhi za Taifa hayafikiki kwa
urahisi kutokana na ubovu wa viwanja vya ndege na barabara. Hivi sasa, changamoto
hii inaongeza ugumu wa usimamizi wa maliasili ndani ya hifadhi za Taifa na usafiri wa
watalii. Hivyo, hatua hii ya Serikali itaongeza idadi ya watalii na hivyo mapato
yatokanayo na shughuli za utalii.

Serikali kupitia Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, imeandaa mikakati ya


kuboresha uwanja wa ndege wa Nduli uliopo Iringa, na barabara za kuingia hifadhini
hususani barabara ya Iringa – Ruaha. Hatua hii, itaunganisha Mkoa, Hifadhi za Taifa na
vivutio vingine vya utalii..

Mheshimiwa Makamu wa Rais,

Hifadhi za Taifa zinakabiliwa na migogoro na wananchi wanaozunguka hifadhi kutokana


na uvamizi wa maeneo ya hifadhi au wanyamapori kuvamia maeneo ya wananchi.
Mradi wa REGROW utafungua fursa za utalii na kuongeza fursa za kiuchumi kwa
wananchi wanaoishi kandokando ya hifadhi, hivyo kupunguza migogoro kati ya
wananchi na wanyamapori. Shughuli za kiuchumi kama vile kilimo cha mbogamboga
kwa ajili ya hoteli zilizoko nje na ndani ya hifadhi, shughuli za utalii wa utamaduni
zitaimarishwa, utengenezaji wa bidhaa za mapambo kwa ajili ya watalii na kufadhili
mafunzo ya hotelia, huduma za ukarimu na kuongoza watalii kwa vijana kutoka katika
vijiji vinavyozunguka hifadhi.

Mheshimiwa Makamu wa Rais,

Mradi huu utagharimu jumla ya Dola za Marekani Milioni 150 ambazo ni sawa Shilingi
bilioni 340. Aidha, Mradi utatekelezwa kwa muda wa miaka sita kuanzia mwaka huu wa
fedha 2017/2018. Kwa heshima na taadhima naomba sasa nikukaribishe uweze
kuongea na wananchi.

Mheshimiwa Mgeni Rasmi, mama yetu Samia Suluhu Hassan, Makamu wa Rais, wa
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, KARIBU SANA.

You might also like