You are on page 1of 4

HOTUBA YA DKT. ALOYCE K.

NZUKI, NAIBU KATIBU MKUU,


WIZARA YA MALIASILI NA UTALII AKIFUNGUA WARSHA YA
KUKUSANYA MAONI YA WADAU KWA AJILI YA KUPITIA UPYA
SERA YA TAIFA YA UTALII YA MWAKA 1999,
DODOMA TAREHE 24 AGOSTI, 2017

Ndugu,
Katibu Tawala Mkoa wa Dodoma,
Kaimu Mkurugenzi wa Utalii,
Mtaalamu Mwelekezi,
Wawakilishi wa Asasi mbalimbali za Sekta ya Utalii Kanda ya
Kati,
Wageni waalikwa,
Mabibi na Mabwana,

Ninayo furaha kubwa kujumuika pamoja nanyi leo katika warsha hii
muhimu ya kuendeleza mchakato wa kupitia upya Sera ya Taifa ya Utalii
ya mwaka 1999. Napenda kuchukua fursa hii kuwapongeza wote
mnaoshiriki warsha hii iliyoandaliwa mahsusi kwa ajili ya kukusanya maoni
yatakayojumuishwa katika Sera mpya ya Taifa ya Utalii. Ni matumaini
yangu kuwa mtashiriki kikamilifu kutoa maoni yenu ili tuweze kuwa na dira
nzuri ya sekta hii yenye mchango mkubwa katika ukuaji wa uchumi wa
taifa letu. Ninatambua kuwa, warsha hii imeshirikisha wadau wa utalii
kutoka mikoa minne ya Kanda ya Kati ambayo ni; Dodoma, Morogoro,
Singida na Tabora.

Nichukue fursa hii kipekee, kuwashukuru wadau wetu wakubwa wa


maendeleo Benki ya Dunia (WB) chini ya uratibu wa Ofisi ya Waziri Mkuu,
1
kwa kutoa ushirikiano wa kuwezesha warsha hii katika kanda mbalimbali
ikiwemo kanda ya Kati ambayo inafanyika leo hapa Mkoani Dodoma.
Aidha, nawashukuru pia wadau wa Sekta Binafsi Shirikisho la Vyama vya
Utalii Tanzania (TCT) kwa kuwezesha warsha kama hii kufanyika Mkoani
Arusha. Ushirikiano wa namna hii ndio utawezesha kuendeleza sekta ya
Utalii na Ukarimu kwa kiwango stahiki na hivyo kukuza uchumi wa taifa
letu.

Ndugu Washiriki,
Ikumbukwe kuwa, Sera ya Taifa ya Utalii iliyopo ilifanyiwa mapitio kwa
mara ya mwisho mwaka 1999 ambapo ni takribani miaka 18 iliyopita.
Katika kutambua hilo, Wizara imeanza kupitia upya Sera hii ili kuhakikisha
Sekta ya Utalii inakidhi changamoto zinazotokana na mabadiliko
mbalimbali yanayotokea duniani yakiwamo ya teknolojia, kijamii,
kiuchumi, kisiasa na mazingira.

Aidha, misingi ya kuandaa Sera nzuri yeyote ni pamoja na kushirikisha


wadau wote muhimu ambao ndio watekelezaji wa Sera hiyo. Tukizingatia
kwamba kuwa Sekta ya Utalii inaendeshwa kwa kiasi kikubwa na Sekta
Binafsi katika kutoa huduma na kufanya biashara za utalii hapa nchini,
tunategemea kupata maoni na michango yenye tija itakayowezesha
upatikanaji wa Sera bora itakayoleta ufanisi katika uendeshaji wa huduma
zinazotolewa katika sekta hii. Kwa kutambua mchango wa utalii kwa
maendeleo endelevu ya taifa letu, ni wazi kuwa tunahitaji Sera wezeshi
yenye kutoa mwongozo wa utaratibu bora na sahihi wa usimamizi,
uendelezaji na utendaji katika sekta ya utalii nchini.

2
Ndugu Washiriki
Ili nchi ifaidike na biashara ya utalii ni lazima wananchi wake wengi kadiri
inavyowezekana washiriki kwenye biashara ya utalii. Hivyo, tunahitaji Sera
ya Utalii itakayowezesha ushiriki wa wananchi wetu katika biashara hii,
hususan katika ngazi ya biashara ndogo na za kati (SMEs), katika Sekta ya
utalii.

Sambamba na msukumo huo wa ushiriki wa wananchi katika biashara hii,


tunahitaji Sera ambayo itaelekeza na kuwezesha kutanua wigo wa mazao
ya utalii, hususan utalii wa maji (pamoja na fukwe), utalii wa mikutano na
matukio, utalii wa utamaduni, ikiwa ni pamoja na utalii unaohamishika na
usiohamishika, na utalii wa historia.

Aidha, tunahitaji kufungua maeneo mbalimbali ya nchi kuweza


kuembelewa na watalii. Hivyo, Sera inayoandaliwa iwezeshe kufungua
maeneo mbalimbali ya nchi, ikiwa ni pamoja na kuanzishwa kwa maeneo
maalum ya uchumi (Special Economic Zones) katika Utalii. Vile vile,
tunataka Sera ambayo itaimarisha ushiriki wa Sekta ya Umma katika
biashara ya Utalii, mahali ambapo Sekta binafsi bado ni changa (kama
ilivyo kwenye usafiri wa anga kimataifa), na pia mahala ambapo Serikali
inaweza kupata mapato zaidi yasiyo ya kodi (non-tax revenue).

Ndugu washiriki,
Wote tunaelewa ya kuwa sekta ya Utalii ni moja wapo ya sekta zinazokua
kwa kasi na hivyo kuchangia kwa kiasi kikubwa ukuaji wa uchumi wa nchi.
Takwimu zilizopo zinaonyesha kuwa, sekta ya utalii inachangia 17.5% ya
Pato la Taifa (GDP) na huliingizia Taifa fedha za kigeni (asilimia 25).

3
Ukuaji wa sekta hii, umedhihirika pale ambapo katika miaka ya hivi
karibuni mapato yatokanayo na utalii yaliongezeka kutoka Dola za
Kimarekani bilioni 1.7 mwaka 2012 hadi kufikia Dola za Kimarekani bilioni
2.1 mwaka 2016. Ongezeko la mapato hayo ni kutokana na kuongezeka
kwa idadi ya watalii kutoka 1,077,058 mwaka 2012 hadi kufikia watalii
1,284,279 mwaka 2016.

Ukuaji huu wa sekta ya utalii umechangiwa kwa kiasi kikubwa na juhudi za


Serikali katika usimamizi, uhifadhi na matumizi endelevu ya rasilimali,
utangazaji, mazingira bora ya uwekezaji pamoja na ushirikiano madhubuti
baina ya sekta za umma na binafsi kwa kuzingatia kanuni na taratibu
zilizopo. Hata hivyo ukuaji huu hauwiani na rasilimali nyingi tulizonazo
ambazo ni nzuri, na za kuvutia ukilinganisha na nchi washindani. Hivyo,
tunapaswa sasa tukae pamoja tujadili na kutoa michango yetu ya dhati
itakayotuwezesha kupata dira ya kutuongoza katika kuinua mchango wa
sekta hii na hivyo kukuza uchumi wa nchi yetu.

Ndugu washiriki,
Tuna kazi kubwa iliyoko mbele yetu, ni vyema sasa kuweka mawazo yetu
kwa pamoja katika kipindi cha masaa machache yajayo na kuibuka na
maoni mazuri yatakayojumuishwa kwenye Sera mpya ya Taifa ya Utalii.

Baada ya kusema haya machache, ninayo furaha kutamka kuwa Warsha


hii ya kukusanya maoni ya wadau wa kanda ya Kati kwa ajili ya kupitia
upya Sera ya Taifa ya Utalii ya mwaka 1999, imefunguliwa rasmi.

AHSANTENI SANA KWA KUNISIKILIZA NA NAWATAKIA


MAJADILIANO MEMA

You might also like