Professional Documents
Culture Documents
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli leo
tarehe 17 Februari, 2020 amezindua kipindi cha 2 cha awamu ya 3 ya mpango wa
kunusuru kaya masikini wa Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF III), katika ukumbi
wa Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Julius Nyerere Jijini Dar es Salaam.
Mhe. Rais Magufuli amebainisha kuwa juhudi za kukabiliana na umasikini hapa nchini
ikiwemo mpango wa TASAF zimepata mafanikio makubwa ambapo takwimu za Ofisi
ya Taifa ya Takwimu zimeonesha kuwa kati ya mwaka 1990/91 na 2017/18 umasikini
wa mahitaji ya msingi (Basic Needs) umepungua kutoka asilimia 39.0 hadi 26.4,
umasikini wa chakula umepungua kutoka asilimia 19.7 hadi 9.5, na kwamba takwimu za
Benki ya Dunia zinaonesha kuwa Tanzania ni nchi inayoongoza kwa kasi kubwa ya
kupambana na umasikini kati ya nchi za Afrika zilizopo kusini mwa Jangwa la Sahara.
Amebainisha kuwa utekelezaji wa TASAF ulioanza mwaka 2000 na ambao kwa sasa
upo katika awamu ya 3 na utagharimu shilingi Trilioni 4.109 zikiwemo shilingi Trilioni
2.032 za kipindi cha pili cha awamu ya tatu amepangwa kunufaisha Halmashauri zote
185 za Tanzania Bara na Wilaya 11 za Zanzibar, na kwamba baada ya kufanya
maboresho sasa ruzuku imepunguzwa kutoka asilimia 67 hadi 38 na itaelekezwa kwa
wazee wasiojiweza, watoto wadogo na kwa wenye kiwango kikubwa cha ulemavu.
Amesisitiza kuwa licha ya kuwa sehemu ya fedha hizo ni ufadhili, sehemu kubwa
ambayo ni kiasi cha shilingi Trilioni 1.035 ni mkopo kutoka Benki ya Dunia na hivyo
amewaagiza viongozi wote wa Mikoa, Wilaya na Halmashauri kuhakikisha
wanasimamia utekelezaji mzuri wa mpango huo na kwamba kufanikiwa ama
kutofanikiwa kwake itakuwa ni kipimo cha kama wanastahili kuendelea na nyadhifa zao
ama laa.
Gerson Msigwa
Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, IKULU
Dar es Salaam
17 Dar es Salaam.