You are on page 1of 1

Bwana Yesu asifiwe milele!

Leo tuangalie faida ya 3 ya kuombea akili za mtu. Faida hiyo ya 3 ni:


“Mungu azisaidie akili zako, ziwe na hali ambayo hatazikataa bali atazikubali”.
Mungu anasema hivi: “Nitaiharibu hekima yao wenye hekima, na akili zao wenye akili
nitazikataa” (1 Wakorintho 1:19).
Mungu anapozikataa “akili zao wenye akili”, ina maana hatashirikiana nazo katika
utendaji wake! Mtu mwenye akili hizo, anaweza kuendelea kuzitumia akili hizo,
lakini ya kwamba, atafanya akifanyacho, bila Mungu kuhusika na afanyacho, na bila
Mungu kuwa upande wake, kwenye hicho afanyacho!
Zipo sababu kadhaa, zinazoweza kumfanya Mungu, azikatae “akili zao wenye akili”.
Lakini kufuatana na mstari tuliosoma hapa juu, tunaona kuwa, aina ya hekima,
inayotoka ndani ya akili, ina uhusiano mkubwa na Mungu kuzikataa akili.
Tukilitazama jambo hili kwa mtazamo huu, tutaona sababu kadhaa zifuatazo,
zinazomfanya Mungu azikatae “akili zao wenye akili”!
Sababu ya 1:
Mungu anazikataa akili zao wenye akili, kwa sababu zinafanya kazi na hekima isiyo
yake! Kufuatana na Ufunuo wa Yohana 17:9, akili zinatakiwa zifanye kazi na hekima
ya Mungu. Hii ni kwa kuwa, akili ziliumbwa na Mungu (Ayubu 32:8), na kwa ajili
hiyo, hekima inayotumika, ni lazima iwe ya Mungu.
Akili ikitumia hekima isiyo ya Mungu, Mungu anaiharibu hekima hiyo, na kuzikataa
akili husika!
Sababu ya 2:
Mungu anazikataa akili zao wenye akili, kwa sababu akili zinatumia “hekima” ambayo
imeuzarau msalaba wa Yesu na kuuona ni “upuuzi” (1 Wakorintho 1:22, 23).
Akili haifanyi sawa kushirikiana na hekima, inayodharau na kupuuzia msalaba wa
Yesu, wakati biblia inasema msalaba huo ni “nguvu ya Mungu, na hekima ya Mungu” (1
Wakorintho 1:24).
Akili inapotumia hekima ya namna hii – kama ya Wayunani, Mungu anaiharibu hekima
hiyo, na kuzikataa akili zao wenye akili, zilizobeba na kutumia hekima hiyo.
Sababu ya 3:
Mungu anazikataa akili zao wenye akili, kwa sababu hazimpi Yesu nafasi
anayostahili, kama msingi wa maisha ya kila siku ya mtu, na msingi wa kazi za kila
siku za mtu.
Biblia inatujulisha ya kuwa, Mungu aliiweka misingi ya nchi kwa kutumia hekima yake
(Mithali 3:19). Na kwa ajili hiyo, akili za mtu zinatakiwa zimpe Yesu, nafasi ya
kuwa msingi wa kila eneo la maisha ya mtu. Hii ni kwa kuwa, msalaba umemfanya Yesu
awe “kwetu hekima itokayo kwa Mungu” (1 Wakorintho 1:30). Na kwa sababu hiyo,
chochote ukifanyacho bila kutumia hekima ya Yesu, hakitakuwa na msingi imara.
Sababu ya 4:
Mungu anazikataa akili zao wenye akili, pale zisipotoa nafasi, kwa hekima ya Mungu
itumike kumsaidia mtu: Kujua wakati wa kuongea; kujua namna ya kuongea; na kujua
wakati wa kunyamaza kimya.
Biblia inasema: Mungu anawapa watu wake, “Kinywa na hekima” (Luka 21:14), ili wajue
cha kusema, na wakati wa kusema, na namna ya kusema.
Lakini pia, biblia inatujulisha ya kuwa, kuna “kunyamaza” ambako ni matokeo, ya
hekima ndani ya mtu, inayomsukuma anyamaze asiongee!
Imeandikwa hivi: “Laiti mngenyamaza kabisa! Hilo lingekuwa hekima kwenu” (Ayubu
13:5).
Kumbuka: Unapoombea Mungu azisaidie akili zako, ziwe na hali ambayo hatazikataa,
bali atazikubali, usisahau kuomba toba kwake, ikiwa mojawapo ya sababu hizo nne,
inakuhusu, au zote zinakuhusu.
Hii itampa Mungu nafasi ya kukusamehe, na kujibu maombi haya juu ya akili zako!

You might also like