You are on page 1of 2

Bwana Yesu asifiwe milele.

Tuendelee na somo letu lenye kichwa hiki: KETI PAMOJA NA YESU KRISTO UBADILIKE
UNAVYOISHI KWA KUBADILIKA UNAVYOFIKIRI.
Leo, nataka tuangalie jinsi “kuketi kwenye nafasi kulivyo na sauti juu ya
“kufikiri”, kwa huyo aliyeketi katika nafasi hiyo; na jinsi kufikiri kwake kulivyo
na sauti juu ya aina ya maisha yake, aliyonayo na anayokuwa nayo!
Hebu tutafakari kwa pamoja, mfano huu ufuatao: Fikiria mtu aliyekuwa mkurugenzi wa
idara katika kampuni moja, anapoamua kuacha kazi, na kuhamia kampuni nyingine. Na
kwenye kampuni nyingine aliyohamia, anapewa kazi ya kuwa Mkurugenzi mkuu wa kampuni
hiyo.
Lakini, pia, inawezekana kabisa ya kwamba, mtu aliyekuwa mkurugenzi wa idara katika
kampuni moja, akapanda cheo au akapandishwa cheo, na kuwa Mkurugenzi mkuu wa
kampuni hiyo hiyo.
Ukifuatilia maisha ya mtu kama huyo, huoni kwa haraka maisha yake yakibadilika.
Lakini baada ya muda kupita, utaanza kuona mabadiliko katika maisha yake.
Utaona jinsi ambavyo kuongea kwake kulivyobadilika, na jinsi anavyoishi
alivyobadilika. Utaweza kuona jinsi ambavyo watu walio karibu naye, wamebadilika na
si wale waliokuwa karibu naye kabla hajapanda cheo!
Lakini utaona pia ya kuwa, jinsi anavyoamua, amebadilika! Na utaona jinsi
vipaumbele vya matumizi yake ya fedha, vilivyobadilika! Na kuongea kwake kunakuwa
na mamlaka ya Mkurugenzi mkuu, na si mamlaka ya mkurugenzi wa idara!
Mabadiliko hayo yametokana na nini? Hayo mabadiliko yanatokana na sababu ya kwamba,
“kufikiri kwake kumebadilika, na mabadiliko hayo ya kufikiri, ndiyo yaliyosababisha
mabadiliko ya maisha yake”.
Biblia inasema hivi: “Maana aonavyo nafsini mwake, ndivyo alivyo” (Mithali 23:7a).
Tafsiri nyingine ya kibiblia ya mstari huu, inasema hivi: “Maana afikirivyo nafsini
mwake, ndivyo alivyo”!
Hii ina maana ya kuwa, alivyo mtu kimaamuzi, au kimaisha, au kimaongezi, au
kimarafiki, au kimatumizi ya muda, au matumizi ya fedha; ni matokeo ya aonavyo, au
afikirivyo nafsini mwake!
Hiki kilichotokea kwa mtu huyo “alipoketi” kwenye kiti cha (au nafasi ya)
Mkurugenzi mkuu, ndicho kinachotokea mtu “anapoketi” kwenye kiti cha (au nafasi ya)
Yesu Kristo “pamoja na Kristo”!
Biblia inatujulisha ya kuwa: “Lakini Mungu, kwa kuwa ni mwingi wa rehema, kwa
mapenzi yake makuu aliyotupenda; hata wakati ule tulipokuwa wafu kwa sababu ya
makosa yetu; alituhuisha pamoja na Kristo; yaani, tumeokolewa kwa neema. Akatufufua
pamoja naye, akatuketisha pamoja naye katika ulimwengu wa roho, katika Kristo Yesu”
(Waefeso 2:4 – 6).
Kwa muhtasari, Waefeso 2:4 – 6 inatujulisha ya kuwa, upendo wa Mungu ulipotuokoa,
ulituketisha pia pamoja na Kristo Yesu!
Mkurugenzi wa idara alipopandishwa cheo, na kuketishwa kwenye nafasi ya mkurugenzi
mkuu, kulitokea mambo kadhaa katika kufikiri kwake, kulikotumika kubadili maisha
aliyokuwa nayo.
Jambo la 1: Mkurugenzi huyo alipopanda cheo, alibadilika ALICHOKUWA ANAFIKIRI, na
alibadili ALICHOKUWA ANAONA!
Hii ni kwa sababu ndani ya “nafasi” ya “cheo” cha Mkurugenzi Mkuu, alisoma vitu
vipya na aliona vitu vipya, ambavyo havipatikani kwenye nafasi ya cheo kingine,
isipokuwa hicho cha Mkurugenzi mkuu wa kampuni hiyo. Vitu hivyo viliwekwa ili
vimsaidie “awe” Mkurugenzi Mkuu kama inavyopaswa Mkurugenzi mkuu “awe” kwa njia ya
kufikiri!
Vivyo hivyo, kinachotokea unapookoka kwa njia ya Yesu Kristo, ni kwamba unafufuliwa
pamoja na Kristo, na unaketishwa pamoja na Kristo Yesu!
Nafasi hii ya “kuketi” pamoja na Yesu Kristo ina jukumu mojawapo la kukusaidia,
ubadilike UNACHOFIKIRI na ubadilike UNACHOONA
Hii ni kwa sababu hapo katika nafasi tunayoketi pamoja na Kristo, katika ulimwengu
wa roho; pana vitu ambavyo ni “halali” kwa ajili ya yule aliyeketi hapo pamoja na
Kristo. Vitu hivyo havipatikani katika nafasi ya cheo kingine, isipokuwa hicho cha
Yesu Kristo “Katika ulimwengu wa roho” (Waefeso 2:6).
Vitu hivyo vilivyo “katika Kristo Yesu” vimewekwa na Yesu kutoka msalabani, kwa
njia ya kufufuka kwake, ili vimsaidie ye yote anayekubali kuketi naye, hapo
alipoketi, “awe” jinsi ambavyo anataka “awe” katika Kristo Yesu, kwa njia ya
“kufikiri”, au kwa njia ya kuvifikiria!
Ndiyo maana imeandikwa ya kuwa: “Basi mkiwa mmefufuliwa Pamoja na Kristo,
yatafuteni yaliyo juu Kristo aliko, ameketi mkono wa kuume wa Mungu (Wakolosai
3:1).
Mstari huu wa Wakolosai 3:1 unatujulisha wazi ya kuwa, yapo yanayotuhusu hapo
alipoketi Kristo, tuyatafute yaani tuwe na kiu ya kuona tunayapata! Tutayapata kwa
njia gani? Tutayapata kwa njia ya kuyafikiri!
Ndiyo maana mstari unaofuata wa Wakolosai 3:2 unasema: “Yafikirini yaliyo juu, siyo
yaliyo katika nchi” Hii inatupa kujua ya kuwa, kwa njia ya kufikiri, tunayapata
hayo tuliyoyatafuta na “kuyaona” hapo “juu Kristo aliko” alikoketi “mkono wa kuume
wa Mungu” (Wakolosai 3:1).
Jambo la 2:
Mkurugenzi yule alipopata cheo, na akaketi katika nafasi ya Mkurugenzi mkuu wa
kampuni, alitumia uwezo uliomo katika nafasi hiyo, kubadilika jinsi alivyokuwa
anafikiria kile alichokuwa anafikiria!
Uwezo huo uliomo katika “nafasi” hiyo aliyopewa ulimpa kubadilika alivyokuwa anaona
alichokuwa anakiona. Na alibadilika jinsi alivyokuwa akisikia, alichokuwa
anakisikia!
Mabadiliko hayo – ya alivyokuwa anafikiri; na – ya alivyokuwa anaona; na – ya
alivyokuwa anasikia; ndiyo yaliyobadili maisha yake!
Mabadiliko hayo yalibadili kuishi kwake, na kusema kwake, na marafiki zake, na
maamuzi yake!
Ndiyo maana – biblia inasema ya kuwa: “Maana aonavyo nafsini mwake, ndivyo alivyo”
(Mithali 23:7a)
Vivyo hivyo, kwa yule aliyeketi “kwa Imani” pamoja na Kristo, atapata mabadiliko
juu ya ANAVYOFIKIRIA, na AONAVYO, na ASIKIAVYO. Na maisha yake yatabadilika na
yatafanana na kile alichopangiwa “awe” ndani ya Kristo, kimaisha na kihuduma!
Kumbuka ya kuwa – nafasi (au cheo) inampa uwezo mtu aliyeketi hapo, awe anatafsiri
na kuamua mambo, kwa kufuatana na jinsi hiyo nafasi, inavyompa uwezo wa kutafsiri
na kuamua!
Somo litaendelea siku nyingine. Tuzidi kuombeana. Usiache kumshirikisha mwingine,
somo hili la leo.

You might also like